Loading...

MADIWANI SONGEA WATAKA MKUTANO WA DHARURA KUNG'OA MSTAHIKI MEYA


MADIWANI kumi kati ya madiwani ishirini na nane (28) wa halmashauri ya manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wamemwandikia barua mkurugenzi wa halmashauri ya manispaa hiyo ya kumtaka aitishe kikao cha baraza chenye madhumuni ya kutokuwa na imani na mstahiki meya wa manispaa hiyo Charles Mhagama kwa sababu mbalimbali ikiwemo ya kuchukua gari la halmashauri lenye namba za usajili      SM 3863 aina ya Toyota Cruiser alilokabidhiwa kutokana na nafasi yake na kwenda nalo Mbinga kwenye shughuli zake binafsi ambako gari hilo liliharibika na kuisababishia halmashauri hiyo kugharimia fedha nyingi kwa ajili ya matengenezo.

Akizungumza mjini Songea diwani wa kata ya matarawe (CCM) James Makene alisema kuwa tayari madiwani kumi wamejiorodhesha majina yao na kuambatanisha barua kwa mkurugenzi wa manispaa hiyo yenye kumbukumbu namba MD/SO/013 ya tarehe 15.03.2013 ya kumuomba aandae mkutano maalumu wenye madhumuni ya kutokuwa na imani na meya wa manispaa hiyo.

Alisema kuwa sababu zilizowafanya baadhi ya madiwani waone umuhimu wa kuomba mkutano maalumu ni kwamba mstahiki meya Charles Mhagama inadaiwa kwa muda wote kutumia nafasi yake vibaya kinyume na kanuni za serikali za mitaa (Mamlaka za miji- Maadili ya Madiwani za mwaka 2000)

Alifafanua kuwa tuhuma zingine zinazomkabili mstahiki meya Mhagama ni kwamba alilidanganya baraza la madiwani lililofanyika Oktoba 30 mwaka jana kuwa kuna waraka unaozuia kamati ya maadili ya taarifa inayomhusu kutojadiliwa kwenye baraza la madiwani huku akijua kuwa hakuna waraka kama huo.

Alieleza zaidi kuwa mstahiki meya Mhagama ambaye pia ni diwani wa kata ya Matogoro anatuhumiwa kushiriki vitendo vya rushwa kwa kuchukua fedha kutoka kwa kila mkandarasi anayeomba nafasi ya kutaka kufanya kazi kwenye manispaa hiyo.

Alisema kuwa inadaiwa kuwa alichua rushwa kutoka kwa mfanyabiashara mmoja ambaye hakutaka kumtaja jina na kumruhusu ajenge kibada cha biashara kwenye eneo lisiloruhusiwa na idara ya mipango miji jambo ambalo ambalo linaonekana kuleta utata mkubwa na anadaiwa kuvuruga michoro ya kituo kipya cha mabasi cha msamala iliyochorwa mwaka 2005 ambayo ilionyesha kuwa na vibanda vya maduka thelathini, 27 vibanda vya kukatia tiketi za mabasi lakini hivi sasa vibanda vilivyopo vinafikia tisini na nane na kwamba zoezi zima la ugawaji wa vibanda hivyo ulisimamiwa nay eye mwenyewe na kujipatia fedha kutoka kwa waombaji mbalimbali.

Alisema kutokana na hali hiyo, madiwani kumi wanapinga vikali matendo yote aliyoyafanya mstahiki meya Charles Mhagama na kuamua kujiorodhesha majina ya madiwani na kutia saini kwa kila diwani na kwamba lengo kubwa ni kutaka manispaa hiyo inafanya kazi kwa misingi ya utawala bora.

Kwa upande wake mkurugenzi wa halmashauri ya manispaa ya Songea Nachoa Zakaria alikiri kupokea barua ya madiwani kumi ya kuomba mkutano maalumu wenye lengo la kutokuwa na imani na mstahiki meya Charles Mhagama ambayo alidai kuwa kwa hivi sasa inafanyiwa kazi kwa kuangalia kanuni na sheria kama zitaruhusu kuitisha kikao cha baraza wanachokihitaji madiwani hao.

Hata hivyo ,kurugenzi wa manispaa hiyo Zakaria alisema kuwa madiwani hao walioomba kuitisha kikao cha kutokuwa na imani na meya ni theluthi moja ambayo kisheria haiwezi kutengua nafasi ya meya ila halmashauri inaweza kumwondoa meya madarakani ni theluthi mbili na siyo theluthi moja kwani manispaa ya Songea ina jumla ya madiwani ishirini na nane, na madiwani kumi ndo wamehitaji kikao cha baraza jambo ambalo linaonekana kuwa kinyume na utaratibu lakini bado anaangalia kama kutakuwa na uwezekano wa kuwepo hicho kikao.

Mstahiki meya Charles Mhagama alipohojiwa kwa njia ya simu alisema kuwa mpaka jana alikuwa hajakabidhiwa barua inayomtuhumu kutaka ajiengue katika nafasi aliyonayo kutokana na tuhuma mbalimbali zinazomkabiri licha ya kuwa alidai kuna habari alizozisikia kuwa kuna baadhi ya madiwani wamejipanga kumg’oa katika nafasi hiyo lakini alieleza kuwa ni vyema wafuate sheria na kanuni za kumwondoa madarakani na pia wawe na ushahidi wa kutosha dhidi ya tuhuma wanazozisema kwani endapo barua barua atakabidhiwa atapaswa apewe nafasi ya kuzijibu tuhuma kabla ya kikao cha baraza wanachokihitaji kifanyike na si vinginevyo.




Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top