Loading...

KADA WA CHADEMA AWASIFIA WABUNGE CCM

Na Gideon Mwakanosya- Songea
Mjumbe wa Halmashauri kuu ya Taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Edson Mbogolo, amewamwagia sifa wabunge watatu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) kuwa ndio wawakilishi wazuri na ni wakweli kwa wananchi Bungeni kwani hoja zao wanazozitoa zimekuwa zikileta tija kwa jamii wakiwemo wapiga kura wao.

Hayo yalisemwa juzi (Jumapili) kwenye viwanja vya shule ya msingi Matalawe katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea kwenye mkutano wa hadhara ulioandaliwa na CHADEMA ambao ulihudhuriwa na mamia ya wakazi wa Manispaa hiyo akiwemo Mwenyekiti wa CHADEMA taifa Freeman Mbowe.

Mbogolo aliwataja wabunge ambao alidai kuwa ndio watetezi wazuri wa wapiga kura wao kuwa ni Deo Filikunjombe mbunge wa jimbo la Ludewa mkoa wa Njombe, Kangi Lugola Mbunge wa jimbo la Mwibala mkoa wa Mara na Ally Kessy Mbunge wa jimbo la Nkasi Kaskazini Mkoani Rukwa.

Alisema kuwa kwa muda mrefu amekuwa akiwashangaa wabunge wengi wa CCM ambao wamekuwa wakitoka kwenye majimbo yao kwenda Bungeni bila kubeba hoja za wapiga kura wao badala yake wamekuwa wakitumia muda mwingi kukejeli na kubeza hoja zinazotolewa na wabunge wa upinzani ndani ya Bunge jambo ambalo wanaona ni kitu cha kawaida.
Amewaomba wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania bila kujali itikadi za vyama vyao vya kisiasa ni vyema wawe wanaona ni muhimu kuwa na hoja zitakazoleta manufaa kwa wapiga kura wao na taifa kwa ujumla na si vinginevyo.

Alieleza kuwa inashangaza sana kuona serikali inaacha kuwabana wabunge wanawaobeza wabunge wenzao wanapotoa hoja zenye tija kwa taifa na badala yake serikali hiyo imekuwa ikitengeneza mazingira ya kuwabana wabunge wa vyama vya upinzani na baadhi ya wabunge wa CCM pale wanapotoa hoja Bungeni walizotumwa kutoka kwenye majimbo yao lakini inaanza mikakati ya kuwabana ili wasiendelee kusema ukweli kwa manufaa ya Taifa.

“Ndugu wananchi ninashangazwa kuona kwamba serikali kupitia ofisi ya Bunge ilifikia uamuzi wa kutaka kuwa mijadala inayotolewa Bungeni isirushwe kwenye luninga jambo ambalo linaonesha wazi kuwa serikali haina nia nzuri ya kuhakikisha kuwa wananchi wanaona kinachofanyika Bungeni”. Alisema Mbogolo.

Naye Mwenyekiti wa CHADEMA mkoa wa Ruvuma Joseph Fuime akimkaribisha Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa Freeman Mbowe ili aweze kuongea na wananchi kwenye mkutano huo wa hadhara alisema kuwa CHADEMA mkoa wa Ruvuma kwa sasa hivi imejipanga kikamilifu kuhakikisha kuwa mwaka 2015 majimbo yote ya Mkoa wa Ruvuma yatashikwa na wabunge kutoka CHADEMA na alidai kuwa jitihada zinafanywa zaidi kuhakikisha kuwa jimbo la Songea Mjini, linaloshikiliwa na DK. Emmanuel Nchimbi kwa sasa, ni lazima ushindi wa kishindo upatikane.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa,  Freeman Mbowe, akiongea na wananchi wa Songea alisema kuwa Watanzania wana haki za msingi kuchagua chama cha siasa wanachokipenda ambacho wao wanaona kuwa ndicho kitakachoweza kuwakomboa na si vinginevyo.

Alisema kuwa Tanzania ina makundi mawili ya uongozi ambapo alilitaja kundi la kwanza kuwa ni la viongozi wanaochaguliwa na wananchi wenyewe ambalo linapaswa kuwa na mamlaka na kundi la pili akalitaja kuwa ni la viongozi wanaoteuliwa na Rais ambalo ndilo linaloonekana kusikilizwa zaidi na kuwa na maamuzi makubwa kutoka serikalini hivyo amewataka wananchi waone umuhimu  kwa sasa hivi kuwa viongozi wote wanaoteuliwa na Rais kama vile wakuu wa wilaya na wakuu wa mikoa wanachaguliwa na wananchi na jambo hili liingizwe kwenye katiba mpya.

Alifafanua zaidi kuwa wnanchi katika kila wilaya au mkoa wananchi ni vyema wachague wakuu wa wilaya na wakuu wa mikoa kutoka katika  maeneo yao kupitia kwenye vyama vyao vya siasa badala ya ilivyo sasa hivi ambapo wanateuliwa na Rais kutoka katika maeneo tofauti na wanayoongoza.

Aliwataka Watanzania kutambua kuwa mfumo wa siasa wa vyama vingi sio wa ugonvi wala sio wa kuwekeana chuki badala yake vyama vya upinzani ndivyo vinavyoweka bayana changamoto zilizopo kwa serikali inayoongozwa na chama tawala ambayo inapaswa kuzifanyika kazi changamoto hizo.





Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top