Loading...

UKWELI KIFO CHA KANUMBA: ACP. Charles Kenyela athibitisha kifo cha Steven Kanumba

Na. songeayetu.blogspot.com
Kamanda wa polisi wa mkoa wa kipolisi wa Kinondoni leo mapema asubuhi ameweza kuthibitisha kutokea kwa kifo cha msanii maarufu wa filamu nchini Tanzania Steven Kanumba (Uncle JJ). Kamanda Kenyela alisema kuwa tukio la kifo cha Kanumba limetokea usiku wa kuamkia leo tarehe 7 Aprili 2012. Kutokana kifo hicho cha ghafla cha msanii huyo jeshi la polisi linamshikilia mtu mmoja ambaye inasadikika kuwa alikuwa ni mpenzi wake na marehemu.

Kamanda Kenyela alisema kuwa taarifa za awali zilizopatikana ni kwamba marehemu alimpiga mpenzi wake kutokana na wivu wa kimapenzi ambapo taarifa hizo zilipatikana kutoka kwa ndugu yake marehemu ambaye walikuwa wakiishi pamoja. Baadaye ndugu yake huyo alipofuatilia zaidi alimwona marehemu akiwa katika hali mbaya, na kwenda kutoa taarifa polisi. Kamanda huyo amedai kuwa Polisi walipofika  katika eneo la tukio walimkuta Kanumba tayari ameshakata roho.

Polisi waliweza kuuchukua mwili na kuupeleka hospitali kwa ajili uchunguzi zaidi kuhusiana na tukio hilo. Kuhusiana na undani wa kifo hicho Kamanda ameomba kupewa nafasi zaidi kuhusiana na uchunguzi, kwani taarifa nzuri za kifo hicho zitatolewa na wataalam (madaktari) ambao wanaendelea na uchunguzi na baada ya uchunguzi ataweza kutoa jina la mwanamke ambaye anashikiliwa na jeshi la polisi ambaye ataweza kusaidia kueleza mazingira ya kutokea kwa kifo hicho.

Mwisho, Kamanda Kenyela aliweza kuwapa pole Watanzania wote kwa ujumla na nje ya Tanzania kwa watu wote kutokana na kifo cha msanii ambaye alikuwa kioo cha jamii.



Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top