Loading...

Askari polisi atolewa risasi mbili mwilini

 Na Julius Konala, Songea

ASKARI Polisi PC Lucas Komba aliyejeruhiwa kwa risasi na mkandarasi Joseph Mrema (31) mwishoni mwa wiki iliyopita, mjini hapa, alifanyiwa upasuaji na kuondolewa risasi mbili mwilini.

Mganga Mkuu wa Hospitali ya Misheni Peramiho, Dk. Venance Mushi, amethibitisha kupokelewa kwa mgonjwa huyo na kusema kuwa ameshafanyiwa upasuaji huo na kuondolewa risasi hizo zilizokwama kwenye paja, na sasa anaendelea vizuri.

Alisema kuwa majeruhi huyo alikimbizwa katika Hospitali ya Mkoa wa Ruvuma kwa matibabu, lakini kwa kukosekana vifaa vya kutosha, alipelekwa Hospitali ya Misheni Peramiho iliyoko nje ya mji wa Songea.

Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi George Chiposi alisema tukio hilo lilitokea Mei 20, mwaka huu, majira ya saa 2.45 usiku, maeneo ya Seedfarm katika Manispaa ya Songea, mkoani Ruvuma.

Alidai kuwa mkandarasi huyo alitumia silaha aina ya pisto kufanya unyama huo, baada kuwa amelewa pombe, na hivyo kufyatua risasi hovyo hewani.

Alisema kuwa wakati mkandarasi huyo akifyatua risasi hovyo, askari huyo alimfuata na kumzuia, na ndipo akamfyatulia risasi zilizomjeruhi.

Kaimu kamanda huyo alisema kuwa mtuhumiwa huyo atafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazomkabili baada ya upelelezi wa polisi kukamilika.



Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top