Loading...

MGAO WA UMEME WAWAKERA WANANCHI SONGEA

BAADHI ya wateja wa shirika la umeme Tanzania (Tanesco) wa halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wamelalamikia kutopata huduma ya umeme kwa zaidi ya wiki moja jambo ambalo limesababisha baadhi ya maeneo kwa nyakati za usiku kuwa giza totoro.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti  na waandishi wa habari wakazi hao walieleza adha wanayoipata baada ya Tanesco kushindwa kutoa huduma ya umeme kwenye maeneo wanayoishi ambapo walidai kuwa kuanzia mwanzoni mwa wiki iliyopita hadi sasa umeme haupatikani kabisa hasa katika maeneo ya F.F.U Mahenge,Makambi,Seedfam,Mji mwema  na Matogoro.

Akizungumza kwa jazba Ally Said Mkazi wa Makambi alisema kuwa tatizo la kutokuwepo kwa umeme kunawakwamisha kufanya shughuli zao za kila siku za maendeleo kwani yeye anategemea kupata kipato chake kupitia biashara yake ya  saluni hivyo ameliomba shirika hilo lichukuwe hatua za haraka kurudisha huduma hiyo kwenye eneo la Makam

 Alphonsi Kapinga alisema kuwa shirika la Tanesco ni vyema linapotokea tatizo wakawatangazia wananchi ili waweze kujuwa tatizo kuliko kukaa kimya wananchi wanashindwa kujuwa tatizo ni nini jambo ambalo linawafanya wakose imani na shirika hilo.

Aidha hiyo pia imewakuta akina mama na watoto ambao walikuwa wanaangaika kutafuta huduma ya kusaga nafaka kwenye mashine zinazotumia umeme jambo ambalo limewalazimu kutembea umbali mrefu kwenda kutafuta huduma hiyo na shughuli zingingine za nyumbani kukwama .

 Amina ally mkazi wa F.F.U Mahenge alisema kuwa bajeti ya nyumbani kwake imeongezaka kutokana na kununua baadhi ya mahitaji kama unga ambao ananunua kilo moja sh.1500na mchele kilo moja sh.2500 wakati nyumbani kwake anayo magunia ya mahindi na mpunga ambavyo anashindwa kwenda kusaga kutokana na kukosekana kwa umeme.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Songea  Joseph Mkirikiti alipohojiwa na waandishi wa habari kwa njia ya simu amekiri kuwepo kwa tatizo hilo kutokana na baadhi ya mashine kuharibika na mtaalamu wa kutengeneza mashine hizo muhandisi Steven Manda ambaye pia ni kaimu Meneja wa Tanesco Mkoa wa Ruvuma yupo nje ya mkoa kwa shughuli za kikazi.

Hata hivyo waandishi wa habari walipowasiliana kwa njia ya simu na kaimu Meneja wa Tanesco Ruvuma Mhandisi manada kufuatia kuwepo kwa kero kubwa kwa baadhi ya maeneo mjini Songea alisema kuwa pamoja na kujitokeza kwa tatizo hilo la kutopatikana kwa umeme lakini alidai kuwa yeye si msemaji na badala yake alieleza kuwa msemaji wa shirika yupo makao makuu ya Tanesco jijini Dar es salaam.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma  Said Mwambungu alipohojiwa kwa njia ya simu na mwandishi wa gazeti hili alisema kuwa kweli kuna tatizo la kiufundi kubwa ambalo limejitokeza kwenye mashine za kufua umeme hivyo wamewasiliana na Tanesco makao makuu na tayari wameshatuma mafundi kuja kutengeneza mashine hizo na zitachukuwa siku nne hadi kuja kukaa sawa

Aidha  hivi karibuni serikali ya Mkoa wa Ruvuma pamoja na Wilaya zake ilitangaza mafanikio ya utekelezaji wa ilani ya chama cha mapinduzi (CCM) ndani ya miaka saba kuwa imeweza kuboresha huduma mbalimbali za maendeleo ikiwemo miundo mbinu ya barabara, afya,maji,kilimo ,elimu pamoja na umeme ambao katika manispaa ya Songea ulikuwa sio wa uhakika kwa sababu ya ubovu wa mitambo ya kufulia umeme.



Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top