Loading...

Waliofeli kidato cha nne wapanga kuandamana kumng’oa Kawambwa

WAKATI mjadala wa kushuka kwa kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi wa kidato cha nne ukiendelea nchini, Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa, amemtaka Rais Jakaya Kikwete kuunda tume kuchunguza na kutoa mapendekezo ya mfumo bora wa elimu nchini.
Alisema kwa hali ilivyo sasa mtu mmoja hawezi kujifungia ofisini peke yake na kuja na mfumo wa kuboresha sekta ya elimu utakaokidhi matakwa ya jamii.
Lowassa alitoa kauli hiyo jana wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika ofisini kwake, jijini Dar es Salaam.
Ingawa hakutaka kuzungumzia hoja ya mbunge wa kuteuliwa na Rais, James Mbatia (NCCR- Mageuzi), aliyetaka Bunge liunde kamati kuchunguza udhaifu katika sekta ya elimu na hoja hiyo kutupwa, Lowassa alisema hakuna sababu ya kubishana kama tuna mitaala au la, lakini jambo la msingi ni kuhakikisha tunapata sababu za matokeo mabaya ya wanafunzi wa kidato cha nne.
“Sitaki kuzungumzia mjadala wa bungeni huyo anasema hatuna mitaala, serikali inasema tunayo, hoja ya msingi zaidi ni kuangalia hii mitaala ni sahihi, inatufaa? Mfumo wetu wa elimu ni mzuri?” alisema Lowassa na kuongeza kuwa tume itakuja na majibu kama mitaala yetu ni sahihi na kama inatufaa au la.
Akitolea mfano, Lowassa wakati wa uongozi wa Mwalimu Nyerere, Waziri wa Elimu wakati huo, marehemu Jakson Makweta, aliunda tume kuchunguza mfumo wa elimu na ilikuja na majibu mazuri yaliyofaa kwa wakati ule na sasa tunahitaji tume nyingine kuja na majibu ya wakati uliopo.
“Miaka ya nyuma, Rais Reagan wa Marekani wakati huo, aliunda tume kuchunguza ubora wa elimu inayotolewa nchini mwake na tume hiyo ilikuja na majibu yaliyofanyiwa kazi na leo hii Marekani ina mfumo mzuri na bora wa elimu,” alisema Lowassa.
Alisema matokeo ya kidato cha nne mwaka huu, yanasikitisha na kama taifa lazima tupate sababu za hali hiyo na kutafuta ufumbuzi.
Alitaja baadhi ya changamoto zinazoikabili sekta ya elimu kuwa ni pamoja na kuangalia namna gani serikali inawaangalia walimu kwa maana ya mishahara na mazingira yao ya kuishi wawapo kazini.
“Matokeo ya kidato cha nne yamenisikitisha sana maana asilimia 60 ya wanafunzi kupata ziro ni jambo la hatari. Na napenda kumsihii Rais Kikwete kwamba amefanikiwa sana katika sekta nyingine kama barabara, aunde tume kuchunguza sababu za wanafunzi kufeli, lakini kubwa kuliko zote tume hiyo ije na mapendekezo ya namna bora ya kuboresha mfumo wetu wa elimu,” alisema Lowassa.
Alisisitiza kuwa hoja ya kutaka serikali iunde tume kuboresha mfumo wa elimu, alipata kuitoa mara kadhaa kwani anaamini Elimu Kabla, Kilimo Kwanza.
“Kila Mtanzania anasema lake, wengine wanasema ni hujuma, wengine wanadai kuna mgomo baridi wa elimu, malalamiko na sababu ni nyingi na njia pekee ya kujua ukweli ni kupitia tume,” alisema Lowassa.
Akizungumzia shule za kata alizoziasisi nchini nzima, alisema anajivunia uwepo wa shule hizo hasa kutokana na mwitikio ambao wananchi waliuonyesha wakati anazianzisha.
Alisema matatizo na changamoto zinazozikabili shule hizo ni bora zikatafutiwa ufumbuzi kupitia tume anayopendekeza ianzishwe.
Alisema shule hizo ni mkombozi kwa wananchi wanyonge na zimeleta usawa na ni jambo la kujivunia kwamba ziko kwenye kila kata nchini.
“Hata hivyo kasi ya kuzihudumia shule hizo hatua kwa hatua imepungua na sitaki kumlalamikia mtu, lakini ni bora zikaendelezwa kwa kukabiliana na changamoto zake.
Mbali ya kuzungumzia anguko la elimu, Lowassa pia alizungumzia vurugu za kidini zinazoendelea nchini, hususan kuuawa na kujeruhiwa kwa viongozi wa kidini visiwani Zanzibar.
Aliwasihi Watanzania kutambua kuwa amani iliyopo ina maana kubwa kwani zikianzishwa vurugu za kidini hakuna atakayebaki salama na hakutakuwa na mshindi.
Wakati huohuo, Baraza la Vijana la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), limeitaka serikali kutangaza matokeo ya mitihani ya kidato cha nne yaliyotoka hivi karibuni kuwa janga la kitaifa kwa lengo la kuliepusha taifa na fedheha ya kuzalisha kizazi cha watu wasiosoma.
Mbali na kutaka matokeo hayo kutangazwa kuwa janga la kitaifa, pia baraza hilo limesema limeshaanza kuwasiliana na vijana waliofeli kutoka maeneo mbali mbali ya nchi kwa ajili ya kuandaa maandamano ya kumtaka Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani Taifa (NECTA), Dk Joyce Ndalichako, na Mkaguzi wa Elimu ya Sekondari nchini, waachie nafasi zao kwa madai kuwa wameshindwa kusimamia majukumu yao.
Kauli hiyo iltolewa jana jijini Dar es Salaam, na Katibu Mkuu BAVICHA, Deogratius Mushi, wakati akizungumza na waandishi wa habari na kuelezea kusikitishwa kwao na matokeo ya mitihani hiyo yanayoonyesha asilimia 60 ya wanafunzi, wamepata ziro.
Mushi alisema sababu kuu ya matokeo mabaya ni udhaifu wa serikali kushindwa kusimamia majukumu yake na kuchukulia kila jambo kwa wepesi.
“Hii serikali dhaifu ya CCM, mwaka 2006 ilisema lengo ni kufikia ufaulu wa asilimia 70 wakati huo tukiwa katika asilima 34 leo hata hiyo haipo sasa tunakwenda wapi na jeshi hili kubwa ambalo litakuwa haliajiriki tena kwa kukosa hata sifa ya kuwa na vyeti vya sekondari!?” alisema Mushi.
Katika hatua nyingine kuongezeka kwa idadi ya wanafunzi waliofeli kutasababisha shule na vyuo vingi kukosa wanafunzi.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili kwa kuzungumza na wataalamu wa elimu unaonyesha kuwa idadi kubwa ya wanafunzi watashindwa kujiunga na masomo ya juu pamoja na vyuo.

VIA http://freemedia.co.tz



Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top