Loading...

Saka la madiwani wa Manispaa la kutokuwa na imani na Meya wao laendelea

Na Gideon Mwakanosya,Songea

 MADIWANI wa halmashauri ya Manispaa ya Songea kupitia tiketi ya chama cha mapinduzi wamejikuta wakiwa katika wakati mgumu baada ya kulazimishwa kuorodheshwa majina yao na kuweka saini zao kwa lengo la kuwashinikiza madiwani kumi wa halmashauri hiyo wakiwemo wa chama cha mapinduzi wawili na wa chama cha demokrasia na maendeleo wanane waliomuandikia barua mkurugenzi wa Manispaa hiyo kuomba mkutano maalumu kwa madai kuwa hawana imani na Meya wa halmashauri hiyo Charles Mhagama.

 Baadhi ya madiwani waliojiorodhesha wakiwemo James Makene diwani wa kata ya Matarwe na Joseph Fuime diwani wa kata ya Mjini wameeleza kuwa lengo lao kubwa ni kutaka kuwepo na utawala bora ndani ya halmashauri hiyo kwani Meya wa Manispaa hiyo Charles Mhagama sababu kubwa za kutokuwa na imani naye ni pamoja na kutumia nafasi yake vibaya kwani alichukua gari la halmashauri alilokabidhiwa kutokana na wadhifa alio nao na kwenda nalo wilayani Mbinga kwenye shughuli zake binafsi ambako gari hilo liliharibika gear box na kuisababishia Manispaa hiyo hasara kinyume na kanuni za serikali za mitaa.

Walizitaja sababu zingine kuwa alilidanganya baraza la madiwani la halmashauri ya Manispaa ya Songea lililofanyika Oktoba 30 mwaka 2012 kuwa kuna waraka unaoizuia kamati ya maadili juu ya taarifa zake kujadiliwa kwenye kikao cha baraza la madiwani jambo ambalo halikuwa na ukweli wa aina yoyote.

 Walifafanua kuwa sababu nyingine ni kushiriki vitendo vya rushwa kwa kuchukuwa fedha kutoka kwa kila mkandarasi aliyeomba kufanya kazi kwenye hakmashauri hiyo ili mkataba wake uweze kusainiwa na inadaiwa kuwa alichukuwa rushwa kutoka kwa baadhi mfanyabiashara mmoja ambaye hawakuta kumtaja jina lake  kwenye kituo kikuu cha mabasi cha mjini Songea na kumruhusu kujenga kibanda cha biashara kwenye eneo hilo bila Afisa ardhi kujua wakati akijua kuwa eneo hilo lipo ndani ya kituo cha mabasi.

 Madiwani hao walibainisha zaidi kuwa Meya Charles Mhagama ambaye pia ni diwani wa kata ya Matogoro anadaiwa kuvuruga michoro ya kituo kipya cha mabasi kinachotarajia kujengwa katika eneo la Msamala mjini Songea iliyochorwa na wataalamu wa idara za ardhi na mipango miji mwaka 2005 vikiwemo vibanda 27 vya kukatia tiketi za mabasi kwa sasa hivi vibanda vimefikia mia moja na zoezi zima la ugawaji wa vibanda hivyo linasimamiwa na yeye mwenyewe.

 Walisema kuwa madhumuni makubwa ya kuomba mkutano huyo ni kutokuwa na imani na Mstahiki Meya Mhagama na kwamba maombi ya mkutano maalumu yamezingatia kanuni za kudumu za halmashauri ya Manispaa ya Songea za mwaka 2003 ibara namba 4 na ibara namba 80 na si vininevyo.

 Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea Nachowa Zakaria alipohojiwa na NIPASHE  ofisini kwake kuhusiana na sakata hilo la madiwani kumi kuomba mkutano huo maalumu alikiri kupokea barua yao yenye kumb.MD/ SO/013 ya Machi 15 mwaka huu ambayo imewekwa majina pamoja na saini zao madiwani kumi lakini anajaribu kuangalia kanuni kama zitaruhusu kuitishas mkutano huo walioomba licha ya kuwa kanuni inasema kuwa halmashauri inayoweza kumuondoa madarakani Meya ni theluthi mbili ya madiwani na siyo theluthi moja ya madiwani walioomba mkutano huo.

  Mkurugenzi Zakaria alisema kuwa halmashauri hiyo ina madiwani ishirini na nane na kati ya hao madiwani nane ni wa kupitia tiketi ya chama cha demokrasia na maendeleo huku madiwani wengine wakiwa ni wa chama cha mapinduzi jamba linalonekana kuwa na mvutano mkubwa wa kisiasa.

Hata hivyo NIPASHE iliwasiliana na Mstahiki Meya Charles Mhagama kwa njia ya simu na alipoulizwa juu ya sakata hilo alisema kuwa barua hiyo alikuwa bado hajaipata licha ya kuwa alishapewa taarifa na mkurugenzi wa halmashauri hiyo kuwa kuna barua ya baadhi ya madiwani ya kuomba mkutano maalumu ambayo ilikuwa ina tuhuma zinazomhusu lakini alihitaji kupewa nafasi ya kuziona tuhuma hizo na kuzitafutia majibu.

 Akizungumzia sakata hilo katibu wa chama cha mapinduzi wa wilaya ya Songea mjini Getruda Lupola aliiambia NIPASHE kuwa ofisi yake imesikia taarifa hiyo ya kuwa kuna baadhi ya madiwani wameomba mkutano maalumu lakini alikanusha kuwa hahusiki kwa lolote kuhusu mpango wa kuwasainisha madiwani wa chama cha mapinduzi katika orodha hiyo.



Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top