Loading...

Sugu ang’aka Songwe kuitwa JK

 
                      Joseph Mbilinyi (MB)

MBUNGE wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi (CHADEMA) amesema haungi mkono pendekezo la Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Mbeya kutaka kuuita Uwanja wa Ndege wa Songwe jina la Rais Jakaya Kikwete.
Akizungumza na Tanzania Daima jana jijini Dar es Salaam, Mbilinyi maarufu kama Sugu alisema mapendekezo hayo yametolewa na watu wenye kutaka kujipendekeza kwa mkuu wa nchi badala ya kufikiria kuutangaza Mkoa wa Mbeya katika nyanja ya kimataifa.
Alisema Mbeya ina historia ya kutaka kujitangaza kimataifa na uwanja huo ni fursa pekee ya kufikia malengo hayo aliyoeleza kuwa yanataka kufifishwa na wateule wa rais.
“Siungi mkono uwanja kuitwa kwa jina la JK, tunataka jina litakaloasisi uhalisia wa Mbeya nasi tufahamike kimataifa, kamati ya ushauri ya mkoa chini ya Mkuu wa Wilaya ya Mbeya mjini, Norman Sigala ilikurupuka kuleta wazo hilo kabla ya kuwasiliana na wabunge,” alisema.
Alisema hatua hiyo ya Sigala haiwakilishi mawazo ya wananchi bali inawakilisha mawazo ya mtu aliyeteuliwa na kwamba wao wakiwa wawakilishi wa Mkoa wa Mbeya kwa ridhaa ya wananchi hawawezi kukubaliana na suala hilo.
Kauli ya Sugu iliungwa mkono na wabunge wengine wa Mkoa wa Mbeya, ambapo Mchungaji Lukson Mwanjale wa Mbeya Vijijini (CCM) alisema anasikitishwa na hatua hiyo ya kuliwasilisha wazo hilo bila ya kuwashirikisha wabunge.
Alisema wakati wa kikao cha kamati ya ushauri wabunge wengi hawakuwepo na taarifa hizo walizisikia baada ya kusoma kwenye vyombo vya habari.
Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philip Mulugo ambaye pia ni mbunge wa Songwe, aliomba apewe muda wa kutaka kujua sababu zilizoibua wazo hilo.
Wazo la kuuita Uwanja wa Ndege wa Songwe jina la Rais Jakaya Kikwete linazidi kupata upinzani ambapo awali chama cha NCCR-Mageuzi na kile cha PPT Maendeleo kupitia kwa viongozi wa Mkoa wa Mbeya vilipinga wazo hilo.
chanzi:http://freemedia.co.tz



Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top