Loading...

NAPE ARUSHIWA KOMBORA MKOANI RUVUMA

Na Stephano Mango, Songea

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Mkoani Ruvuma kimemtaka Katibu wa halmashauri kuu ya CCM Itikadi na Uenezi Nape Nnauye kuacha kuwadanganya wananchi kwa kuwapa matumaini ambayo yanaendelea kuwatesa kwa sababu ya kuokoa chama ambacho kinaendelea kufa

Wito huo umetolewa jana kwenye mikutano miwili tofauti yenye lengo la kuwahamasisha wananchi kuvua Gamba na kuvaa Gwanda iliyofanyika kwenye Kata ya Msamala na Kata ya Seedfarm na Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Ruvuma ambaye pia Diwani wa Kata ya Mjini Joseph Fuime ambapo katika mikutano hiyo jumla ya watu 60 walijiunga na chama hicho,ambapo kati yao viongozi wanne wa Ccm kata ya Seedfarm walijivua gamba na kuvaa gwanda

Fuime alisema kuwa Chama cha Mapinduzi kimemtuma Nape azunguke nchi nzima na kuendelea kuwadanganya wananchi kwa kutoa maagizo kwa Serikali ambayo imeshindwa kuifikisha nchi kwenye ustawi stahiki miaka 50 tuka tupate uhuru

Alisema kuwa Serikali iliyopo madarakani inaongozwa na Ccm hivyo maneno ambayo anazunguka nchi nzima kuyaongea Nape ni kuwadanganya wananchi kwani alipaswa amwagize Rais Jakaya Kikwete kwenye vikao vyao vya chama na wananchi waone utekelezaji na sio kutoa maagizo ambayo mtekelezaji wake ameshindwa toka alivyokuwa Rais mwaka 2005

Alifafanua kuwa Serikali ya Ccm toka mwaka 2005 hadi sasa imeshindwa kuwakomboa wananchi kutokana na umaskini ambao unawakabili bali kila siku imekuwa ikiwanyang’anya uwezo wa kuyafikia maisha bora kwa kuwapandishia gharama za maisha kupitia mfumuko wa bei na wafanyabiashara wengi wamekuwa wakitoa huduma kwa Serikali na kuwacheleweshea malipo hali ambayo inaendeleza ugumu wa maisha

Alieleza kuwa baadhi ya wafanyabiashara walihifadhi mahindi ambayo yalinunuliwa na Serikali kwenye magodauni yao na wengine waliyasafirisha mahindi hayo kutoka Songea kuyapeleka Makambako na Dar Es Salaam lakini hawajalipwa hadi leo jambo ambalo linaendelea kuwafanya wananchi wa mkoa wa Ruvuma ambao una viwanda vichache kuishi katika maisha magumu

Naye Diwani wa Viti Maalumu wa Chadema Manispaa ya Songea Roda Komba alisema kuwa Chadema ndicho chama chenye dhamira ya kweli ya kuwakomboa Watanzania wote katika lindi la umasikini, ujinga na maradhi hivyo wananchi kuweni makini sana na porojo za Chama cha Mapinduzi kwani hakina jambo jipya watakalowafanyia wananchi kwasababu kwa muda mrefu wamekuwa wakiwaongoza bila kuleta tija.

Komba alisema kuwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi imeshindwa kuwajali wananchi ,wakiwemo wazee kwa muda mrefu kwa kushindwa kuwapatia huduma stahiki za jamii na kuwasababishia kuona maisha ya uzeeni kama ni hatari ambayo inapaswa kuogopwa

Alisema kuwa katika nchi nyingine wazee wanaheshimika na wanapewa huduma za jamii bure ikiwemo matibabu na pensheni kwa wazee bila kujali kuwa ulifanya kazi serikali kwani mchango walioutoa katika ujenzi wa taifa walipokuwa vijana unatosha kuwaenzi wanapokuwa wazee



1 comments:

hakika watanzania sasa wanaanza kufunguka, kama wameweza hata kutambua kazi ya nape inawadanganya japo sina uhakika lakini inakaribia sana na ukweli kwamba katumwa, habari nzuri nimeipenda kwani inatujenga, http://alloyson.blogspot.com

Reply

Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top