Loading...

POLISI YATAKA WANANCHI WAWAPUUZE LAMBA LAMBA

                             JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI

DODOMA ALHAMISI DESEMBA 14, 2012.


Wakazi wa Dodoma wametakiwa kuondokana na dhana potofu inayoenezwa na kundi la kundi la lamba lamba ya kuwaaminisha wananchi hususani wa vijijini kuwa wanauwezo wa kuondoa na kufichua uchawi na washirikina ambao wanadai wanavuta mali za watu wengine kwao na kuwafanya matajiri.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma Kamishna Msaidizi wa Jeshi la Polisi Bw. David Misime ameeleza hayo katika taarifa yake kwa vyombo vya habari ya kutangaza vita dhidi ya kundi la matapeli la lamba lamba lililovamia na kufanya shughuli zake mjini humo.

Akizungumzia kundi hilo Kamanda David Misime alisema kuwa ni kundi la matapeli ambalo limeundwa na wahalifu kwa lengo la kujihusisha na uhalifu wa  utapeli na ulaghai kwa wananchi hususani wa vijijini, ili kujipatia mali, fedha na mifugo ya aina mbalimbali toka kwa wanavijiji.

“Kundi hili ni mkusanyiko wa watu wa jamii tofauti ambao wanatoka maeneo ya Rufiji, Pwani, Tanga na Morogoro ambao wamekuja kuivamia jamii ya watu Dodoma ambayo nayo ina mila na desturi zake katika mambo ya jadi.” Alielezea Bw. David Misime

Alisema kwamba kundi hilo limekuwa likitumia mtindo wa kujifanya kuwa wao ni waganga wa tiba za jadi kwamba wana uwezo wa kutoa vitu vya kichawi  katika majumba ya watu, sehemu za biashara  na pia kufichua  wachawi, vitu ambavyo  hawana uwezo navyo.

Kamanda Misime alieleza kuwa ili mtu akubalike kuwa ni mganga wa tiba za jadi ni lazima afahamike katika eneo analofanyia shughuli zake hizo kuanzia uongozi wa ngazi ya  chini hadi wa juu wa serikali na awe na kibali cha kuendesha tiba hizo kisheria kitu ambacho kundi la lamba lamba hawakidhi matakwa hayo.

Aliongeza kuwa  Mganga wa jadi kwa asili yake hatakiwi kufanya kazi zake kwa kuita  watu ni wachawi bali anapaswa kutoa tiba na kinga kwa kutumia miti shamba kulingana na uwezo wake, na sio wanachofanya hao wanaojiita lambalamba.

Kamanda Misime alisema kundi la lambalamba  kwa kushirikiana na washirika wao, huwa wanapandikiza vitu  kwenye nyumba, mashamba au sehemu za biashara za walengwa nyakati za usiku na baada ya kufanya hivyo ndipo wanaondoka na kundi la watu na kwenda kutoa vitu ambavyo walishavipandikiza kabla.

Alieleza kwamba madhara yanabaki kwa anayefanyiwa hivyo kwa kudhalilika yeye na familia yake kuwa  ni mchawi na kibaya zaidi hulazimishwa kutoa kiasi cha fedha na mifugo kama adhabu na  kutishiwa wasithubutu kwenda kutoa taarifa Polisi.

“Hili ni kosa la jinai na ukiukwaji mkubwa wa haki za Binadamu, hatuwezi kuvumilia na kuwaacha wananchi wenzetu kuendelea kupoteza fedha na mali zao kwa kuwanufaisha hao matapeli.” Alisistiza Bw. David Misime

Aidha aliongeza kwamba zipo taarifa kuwa lambalamba hao wanapofika vijijini hutafutiwa wanawake wa kuwapikia na kisha kuwastarehesha kitu ambacho ni unyanyasaji wa kijinsia na jambo la hatari ambalo linachangia kuenea kwa magonjwa ukiwemo UKIMWI.

Bw. David Misime alisema hayo yanayofanyika ni utapeli mkubwa uliobuniwa na watu hao wa kujipatia fedha na ni jambo linalodhalilisha, linalojenga chuki, na uchochezi ndani ya jamii  na  kuhatarisha usalama, utulivu na  amani pamoja na kuathiri  afya za wanawake na jamii nzima kwa ujumla. 

Kamanda David Misime ametoa wito kwa wananchi kwa  kupitia mkakati wa Polisi Jamii na dhana ya utii wa sheria  kwa hiari kushirikiana kwa pamoja na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za watu  hao ili kuutokomeza uhalifu huu ili jamii iendelee kubaki  salama na inayoweza kufanya shughuli mbalimbali za kujiletea maendeleo.

MWISHO:
CONTACT:
POLISI MKOA WA DODOMA
DAWATI LA HABARI, ELIMU NA MAHUSIANO,
Phone:  0715 006523, Luppy Kung’alo – Mrakibu msaidizi wa Polisi (ASP)
Phone:  0712  360203, Silyvester Onesmo – Police  Konstebo  (PC)



Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top