Loading...

karani wa mahakama kizimbani kwa wizi wa nyara za serikali

KARANI  mmoja  wa mahakama ya mkoa wa Ruvuma amepandishwa kizimbani katika mahakama ya hakimu mkazi wa mkoa wa Ruvuma kwa tuhuma za kuiba nyara za serikali zilizokuwa zimehifadhiwa kwenye stoo ya kuhifadhia vilelezo zenye thamani ya shilingi 962,500.

Ilidaiwa na upande wa mashtaka na mwendesha mashtaka wa serikali ambaye ni mwanasheria wa ofisi ya mwanasheria Kanda ya Songea Tulibake Juntwa mbele ya hakimu mkazi wa mahakama ya mkoa wa Ruvuma Casmil Mwalunyungu kuwa Sadick A. Makundi (49) ambaye ni karani wa mahakama ya mkoa wa Ruvuma anashtakiwa kuwa akiwa mtunza stoo ya mahakama aliiba vipande viine kati ya vipande nane vya meno ya tembo.

Juntwa alibainisha zaidi mahakamani hapo kuwa  tukio hilo lilitokea kati ya Mei 25 mwaka jana na Januari 16 mwaka huu katika majira yasiyofahamika kwenye ofisi ya mahakama ya mkoa wa Ruvuma wakati akiwa mtunza funguo za stoo hiyo.

Alisema kuwa vipande hivyo vya meno ya tembo vilipokelewa mahakamani kama kielelezo cha kesi ya uhujumu uchumi namba 9 ya mwaka 2007 ambayo iliisha Mei 25 mwaka jana ambapo mahakama ilikuwa imeamuru nyara hizo za serikali ziuzwe kwa kupitia idara ya wanyamapori kisha fedha hizo ziingizwe serikalini.

Aidha, mwanasheria huyo wa serikali Juntwa alibainisha zaidi mahakamani hapo kuwa maafisa wa idara ya wanyamapori walipomfuata Makundi ambaye kwa sasa ni mshitakiwa hakutaka kutoa nyara hizo za serikali hadi alipoamriwa tena na hakimu mkadhi mfawidhi wa mahakama ya mkoa wa Ruvuma Frank Mahimbali na kukuta meno 4 kati ya meno 8 hayapo kwenye stoo hiyo wakati funguo za stoo hiyo alikuwa anazo mshitakiwa Makundi.

Hata hivyo, mshitakiwa Makundi baada ya kusomewa shitaka hilo amekana na yuko rumande baada ya kukosa mtu wa kumdhamini hadi Februari 18 mwaka huu kesi itakapotajwa tena na kwamba kesi hiyo inatarajiwa kusikilizwa na hakimu mkazi mfawizi wa mahakama ya wilaya ya Mbinga kwa madai kuwa mshitakiwa ni mtumishi wa mahakama ya mkoa hivyo ni lazima kesi hiyo isikilizwe na hakimu wa mahakama nyingine ili kuepuka malalamiko.



Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top