Loading...

Matokeo kidato cha nne ‘feki’, Mkurugenzi Green Acres afichua siri nzito


na Betty Kangonga
WAKATI mjadala wa matokeo mabaya ya kidato cha nne ukiendelea kulitikisa taifa, kashfa mpya ya matokeo hayo imeibuliwa.
Kashfa hiyo mpya imeibuliwa na Mkurugenzi wa Shule ya Green Acres, Julian Bujugo, kwamba matokeo ya baadhi ya shule nchini ikiwamo yake yamechakachuliwa.
Akizungumza na gazeti hili jana, Bujugo alisema kuwa baadhi ya wanafunzi kwenye shule yake hawakufanya mitihani ya kidato cha nne, lakini matokeo yanaonesha wamefaulu kwa kupata alama za juu.
Alitaja mfano wa mwanafunzi, Humphrey Sanga, mwenye namba 01197/148, ambaye hakufanya mitihani hiyo lakini matokeo yanaonesha amefaulu kwa kupata alama nzuri.
“Huyu mwanafunzi tulimsimamisha na hakufanya mitihani, lakini matokeo yake yanaonekana amepata hivi; Civics D, Historia D, Jiografia C, Kiswahili D, English C, Physics D, Chemistry C, Biology C, Basic Mathematics D, ambapo amepata daraja la tatu pointi 24,” alisema Bujugo.
Alimtaja mwanafunzi mwingine, Martin Rushaigwa, namba 01197/0173, ambaye alifanya masomo ya ‘Arts’.
Alisema matokeo ya mwanafunzi huyo yanaonesha kuwa ameongezewa alama za masomo ya biashara ya Bookeeping na Commerce, ambayo hakuyafanya kabisa.
Alimtaja mwanafunzi mwingine aliyefanya mtihani huo lakini matokeo yake yanaonesha amewekewa ‘absent’ na mwanafunzi mwingine, Mbazi Volta, hakufanya mitihani lakini amepewa alama za ufaulu.
“Matokeo hayo yananipa wasiwasi kwamba yanaweza kuwa yamechakachuliwa,” alisema Bujugo.
Mkurugenzi huyo anaiomba Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kurudia kusahihisha mitihani hiyo ili kuondoa ukungu ulioligubika taifa kwa sasa kuhusu matokeo ya kidato cha nne.
“Naomba usahihishaji urudiwe, maana huu ni ubabaishaji mkubwa…matokeo hayo yamewaathiri watoto kisaikolojia na sijui watakwenda wapi?,” alihoji.
Alisisitiza kuwa usahihishaji urudiwe kwani katika shule hiyo wanafunzi wenye uwezo mkubwa tangu walipoanza kidato cha kwanza ndio waliofanya vibaya wakati waliokuwa wakifanya vibaya, wameibuka na alama za juu.
Mkurugenzi huyo alisema wazazi wa watoto hao wanatarajiwa kukutana mwishoni mwa wiki hii kujadiliana kuhusu matokeo hayo na hatua za kuchukua.
Akitolea ufafanuzi suala hilo, Msemaji wa Baraza la Taifa la Mitihani (NECTA), John Nchimbi, alisema si kweli kuwa matokeo hayo yamechakachuliwa bali ni matokeo halisi ya shule hiyo.
Alisema iwapo mkurugenzi wa shule hiyo ana shaka na matokeo hayo, alitakiwa kufika katika ofisi za baraza hilo ili apatiwe taarifa sahihi kabla ya kutoa taarifa katika vyombo vya habari.
“Mi nimeangalia hayo majina, naona yapo sawa na hata huyo mwanafunzi ambaye anasemekana hakufanya mitihani na akapewa alama…napenda kusema kuwa alama alizopewa si zake na hata katika orodha yetu anaonekana kuwa hakufanya mitihani,” alisema.
Katika hatua nyingine, Waziri wa wizara hiyo, Dk. Shukuru Kawambwa na wenzake, wamekuwa bubu kueleza endapo wako tayari kujiuzulu au la.
Tanzania Daima ilifika wizarani hapo jana kutaka kuonana na Waziri Kawambwa ili atoe msimamo wake, mwandishi alijibiwa kuwa waziri huyo alikuwa kikaoni na asingeweza kutoka.
Hata waziri alipopigiwa simu pamoja na kutumiwa ujumbe mfupi wa maneno, hakupokea wala kujibu ujumbe huo.
Kwa upande wake, katibu mkuu wa wizara hiyo naye hakuwa tayari kuzungumzia suala hilo kwa madai kuwa alikuwa kikaoni.
Naye Naibu Waziri, Philipo Mulugo, alipotafutwa kupitia simu yake ya mkononi kueleza msimamo wake, simu yake iliita bila kupokewa na hata hakuwa tayari kujibu meseji ya ujumbe mfupi.
 
via tanzania daima



Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top