Loading...

LWAKATARE ATUPWA GEREZANI HADI APRIL 3 BAADA YA KUFUNGULIWA MASHITAKA UPYA


MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam imewafutia kesi ya makosa ya ugaidi  Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Wilfred Lwakatare  na Ludovick Joseph baada ya Mkurugenzi wa Mashitaka( DPP), Dk Eliezer Feleshi kuwasilisha hati ya kuwafutia kesi hiyo washitakiwa kwa sababu hana haja ya kuendelea nayo.

Sambamba na hilo, DPP ilimfungulia kesi ya makosa ya ugaidi  upya Lwakatare na Ludovick ambapo kesi hiyo mpya namba  Na.6/2013 ambapo imepangiwa kwa hakimu mpya Aloyce Katemana.

Katika kesi ya ugaidi Na.37/2013 iliyofunguliwa na Jamhuri dhidi ya Lwakatare na wenzake Machi 18 mwaka huu, ambayo ilifutwa saa tatu asubuhi na ambayo ilikuwa imekuja kwa ajili ya Hakimu Mkazi, Emilius Mchauru kuitolea uamuzi wa ama wa kuwapatia dhamana washitakiwa au la, hakimu Mchauru alijikuta akishindwa kutoa uamuzi wake kwa sababu  mawakili viongozi wa serikali Ponsian Lukosi, Prudence Rweyongeza na Peter Mahugo waliwasilisha  hati hiyo ya DPP chini ya kifungu cha 91(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002, ambapo kifungu hicho kina mpa mamlaka DPP, kuifuta kesi yoyote ya jinai muda wowote kabla ya haijatolewa hukumu na uamuzi huo wa DPP haujahojiwa na mtu yoyote.

“Kwa kuwa kesi hii Na.37/2013 ilifunguliwa na upande wa jamhuri MAchi 18 mwaka huu, na leo kesi hii ilikuja kwa ajili ya mahakama kutolea uamuzi wa maombi ya washitakiwa kupatiwa dhamana au la  pamoja na maombi mengine…mahakama hii inasema haitaweza kutoa uamuzi wake kwa sababu DPP amewasilisha hati ya kutotaka kuendelea kuwashitaki washitakiwa  na hivyo mahakama hii inawafutia kesi washitakiwa wote”alisema hakimu Mchauru.

Baada ya hakimu Mchauru kuwafutia kesi, askari kanzu waliwakamata tena washitakiwa hao na kuwaweka chini ya ulinzi wa gari la polisi na ilipofika saa 4:20 asubuhi, washitakiwa hao wakiwa chini ya ulinzi mkali wa wana usalama waliingizwa tena katika ukumbi namba mbili wa mahakama  hiyo mbele ya hakimu mkazi mwingine Aloyce Katemana.

Mawakili Wakuu wa Serikal, Ponsian Lukosi, Prudence Rweyongeza na Wakili Mwanadamizi wa Serikali Peter Mahugo walidai kuwa kesi hiyo nimpya na imepewa Na.6 ya maka huu, ambapo washitakiwa ni Lwakatare na Ludovick wanaotetewa na mawakili wa kujitegemea Profesa Abdallah Safari na Peter Kibatara na kwamba hati hiyo mashitaka ina jumla ya  mashitaka manne ambapo shitaka la kwanza linaangukia kwenye Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002 na makosa matatu yote yanaangukia kwenye Sheria ya Kuzuia Ugaidi ya mwaka 2002.

 Wakili Rweyongeza alililata kosa la kwanza ambalo linawakabili washitakiwa wote kuwa ni la kula njama kutenda kosa la jinai kinyume na kifungu cha 284  cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002 , na kwamba mnamo Desemba 28 mwaka jana, huko Kimara King’ong’o  Stopover, wote kwa pamoja walitenda kosa hilo kwa kutaka kutumia  sumu kwa lengo la kumdhuru  Denis Msaki  ambaye ni Mhariri wa habari wa Gazeti la Mwananchi ambalo ni kinyume na kifungu cha 227 cha sheria hiyo.

Wakili Rweyongeza alilitaja  kosa la pili kuwa ni la kula njama  ambalo pia ni kwaajili ya washitakiwa wote  ambalo ni kinyume na kifungu cha 24(2) cha Sheria ya Kuzuia Ugaidi Na.21 ya mwaka 2002, ambapo washitakiwa hao walitenda kosa la ugaidi la  kutaka kumteka Msaki  kinyume na kifungu  cha 4(2)(c) (iii) cha Sheria ya Kuzuia Ugaidi ya mwaka 2002.

Shitaka la tatu ni la washitakiwa wote ambapo wanashitakiwa kwa kosa la  kupanga kufanya makosa ya ugaidi  kinyume na kifungu cha 59(a) cha Sheria ya Kuzuia ugaidi kwamba Desemba 28 mwaka jana,walishiriki katika mkutano wa kupanga kufanya vitendo vya kumteka nyaraka Msaki  kinyume na kifungu 4(2)(c) (iii) cha Sheria ya Kuzuia Ugaidi.

Shitaka la nne, Rweyongeza alidai linamkabili Lwakatare peke yake  ni kuwezesha kutendeka kwa kosa la ugaidi kinyume na kifungu cha 23(a) cha sheria ya kuzuia ugaidi , kwamba Desemba 28 mwaka jana, Lwakatare akiwa ni mmiliki nyumba hiyo ilipo Kimaraka King’ong’o  kwa makusudi  aliliruhusu  kufanyika kwa kikao hicho baina yake na Ludovick  cha kutenda kosa la ugaidi la kutaka kumteka nyara Msaki hata hivyo walikanusha mashitaka hayo.

Hata hivyo  Hakimu Katemana alisema washitakiwa hao hawatakiwi kujibu chochote kwasababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo na akaiarisha kesi hiyo hadi Aprili 3 mwaka huu, itakapokuja kwa ajili ya kutajwa.

Wakili Kibatala aliomba mahakama isikilize ombi lake alilokuwa akitaka kuliwasilisha, lakini Hakimu Katemana alisema yeye ndiye kiongozi na mawakili wa utetezi, Jamhuri wapo chini yake na akamweleza Kibatala mahakama ni mhimili unaongozwa kwa taratibu zake na nilazima Kibatala azifuate, hivyo, kwa kuwa yeye hakimu ana majukumu mengine, leo hayupo tayari kusikiliza ombi la Kibatala wala ombi la upande wa Jamhuri (lilokuwa linaomba mahakama imruhusu Ludovick aendelee kushikiliwa na jeshi la polisi kwa ajili ya hatua  zaidi za kipelelezi,) na kuamuru washitakiwa wapelekwe gerezani.
Itakumbukwa kuwa Machi 18 mwaka huu, Hakimu Mchauri alitoa fursa kwa washitakiwa ya kukubali au kukanusha mashitaka licha ya Hakimu wa Mahakama hiyo ya Hakimu Mkazi kutokuwa na ruhusa ya kutoa fursa hiyo kulingana na makosa yanayowakabili  watuhumiwa na kwa mujibu wa sheria za nchi.  Mahakama Kuu pekee ndiyo yenye mamlaka ya kusikiliza kesi za  makosa ya tuhuma za ugaidi.

Baada ya kesi hiyo kuairishwa wafuasi wa CHADEMA na watu wengine wakiwa wamevalia sare walipaza sauti na kusema ‘Peoples Power… hakuna kulala hadi kwanza walale wao’.

Hali iliyosababisha wanausalama waliokuwa wamevalia sare na wale waliovalia kiraia waliokuwa ndani ya kumbi wa kesi ilipokuwa ikiendeshewa kuwataka watu wote watoke ndani ya ukumbi huo haraka ili waweze kuwapitisha washitakiwa, amri ambayo wafuasi hao waliitii bila shuruti.

Msafara wa magari nane ukiongozwa na magari ya jeshi la magereza, polisi waliondoka ndani ya viwanja hivyo kwa ajili ya kuwapeleka watuhumiwa katika gereza la Keko , huku askari wa kikosi cha mbwa wakiwa  bado katika eneo la mahakama hiyo kwa ajili ya kuimarisha ulinzi. Hata hivyo, hali ilikuwa ni shwari kwa sababu hakukuwepo na vitendo vya uvunjifu wa amani kwani wafuasi wa CHADEMA waliondoka mahakamani hapo kwa utulivu wa hali ya juu huku wengine wakiangua vilio kwa uchungu.

Mbwa waliokuwepo wakiimarisha ulinzi eneo hilo ni Kino, Pd Kambi Simba, Giro, Pd Roja, Pd Ivo, Pd Undra, Pd Bobi ambao wamepata mafunzo ya kuimarisha ulinzi kutoka nchi mbalimbali ikiwemo Lebanon.

Akizungumza nje ya viwanja vya mahakama  baada ya kesi kuahirishwa, Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe alisema kwanza asingependa kuingilia mtiririko wa mahakama na kuwataka waandishi wa habari wamuhoji wakili wa washitakiwa. 


Akasema wao wanafanyakazi za mageuzi kwa ajili ya kuwatetea raia wanyonge na maskini na kwamba kilichompata Lwakatare siyo geni, bali ni mtiririko wa mabavu ya dola dhidi ya wanamageuzi.

CREDIT: http://freebongo.blogspot.com


Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top