Loading...

Wakazi wa Manispaa ya Songea walalamikia uchafu uliokithiri

Hili ni moja ya Ghuba lililopo pembezoni ya Mjia wa Songea

 
Ghuba hili lipo mtaa wa mahenge ambalo pia limesahulika kuzolewa taka
  Pichani hapo juu ni ghuba lililopo Mtaa wa Sovi barabara iendayo kituo kikuu cha Polisi likiwa limejaa uchafu .
Wafanya biashara wa Mabucha ya Nyama na wauza Viungo wakiendelea na biashara huku pembeni kukiwa na hali ya uchafu uliokithiri wasiwe na wasiwasi.
.......................................................................
Na Nathan Mtega,Songea
 BAADHI ya wakazi wa halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wamelalamikia kukithiri kwa uchafu katika maeneo yote ya Manispaa hiyo na kusababisha maghuba ya kuhifadhia taka kufurika kwa muda mrefu yakiwemo yanayozunguka maeneo ya soko kuu,Majengo na kituo kikuu cha mabasi cha mjini Songea.

 Wakizungumza kwa nyakati tofauti walisema kuwa mazingira ya usafi kwa ujumla katika Manispaa ni mabaya na yanaweza yakaleta madhara makubwa ya kiafya ikiwa hali hiyo haitachukuliwa hatua za haraka na maafisa afya wa Manispaa hiyo kwa sababu baadhi ya maghuba yamefurika na kutoa harufu kali.

 Walisema kuwa ni muda mrefu hali hiyo ya uchafu imeendelea kuwepo na hakuna jitihada zinazofanyika kuiondoa hali hiyo ambayo ni kero kubwa kwa wakazi walio wengi wa Manispaa hiyo licha ya kuwa wamekuwa wakilipa ushuru wa usafi wa mazingira kila mwezi.

 Wakizungumza Sebastiani Komba na Elizabeth Luambano wakazi wa Bombambili walisema kuwa ni vyema halmashauri ya Manispaa hiyo ikachukua hatua za haraka za kuiondoa adha hiyo ambayo imekuwepo kwa muda mrefu huku Adam Haule na Edson Kumbuka wakazi wa Majengo wakisema kuwa maghuba ya kuhifadhia taka yaliyopo yamefurika kupita kiasi na watoto wakicheza kwenye maghuba hayo hali ambayo inaweza ikawasababishia madhara.

 Naye Seleman Said mfanyabiashara wa soko kuu alielezea kusikitishwa kwake na hali ya kukithiri kwa uchafu ndani ya eneo la soko kuu ambamo kuna ghuba la kuhifadhia taka ambalo ni muda mrefu gali la kuzoa taka halijafika kuchukua taka taka zilizofurika kwenye ghuba hilo na Rashid Husein wa kituo kikuu cha mabasi cha mjini Songea alisema kuwa taka taka zilizopo kwenye ghuba ambalo lipo kando kando mwa kituo hicho zimekuwa kero kwa wasafiri na wapiti njia.

 Afisa afya wa Manispaa ya Songea Maxmilian Mahundi alipojohojiwa na mwandishi wa habari kuhusiana na hali hiyo alikataa kusema chochote kwa madai kuwa yeye siyo msemaji hata hivyo jitihada za mwandishi wa habari zilimtafuta Mkurugenzi wa Manispaa ya Songea Nachowa Zacharia ambaye alikiri kukithiri kwa uchafu katika halmashauri hiyo.

 Alisema kuwa halmashauri ya Manispaa ya Songea ina magari mawili tu ambayo ni chakavu na yana zaidi ya miaka ishirini tangu yaliponunuliwa huku mahitaji ya magari mapya kwa ajili ya kuzoa taka ni sita ambayo yana uwezo wa kubeba taka tani ishirini kila moja na kijiko kimoja cha kuzolea taka badala ya kutumia vibarua ambao wamekuwa wakifanya kazi hiyo kwa kutumia vitendea kazi duni.

 Aidha amewahimiza wakazi wa Manispaa kuendelea kulipa ushuru wa usafi kwa kila kaya ambayo ni shilingi 150 kwa kila siku ili kupunguza adha iliyopo ya uchafu uliokithiri kwenye maeneo mengi ya Manispaa hiyo



Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright songeayetu.blogspot.com | Designed By JUNGUKUU.US
Back To Top